Saturday, February 11, 2017

Mabalozi wafunguka kinachowakuna kwa JPM



Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao hapa Tanzania, wamempongeza Rais Magufuli pamoja na serikali ya awamu ya tano kwa jitihada zake za kupambana na rushwa, kujenga nidhamu kwa watumishi wa umma na kuimarisha uchumi.
Akizungumza kwa niaba ya mabalozi wenzake katika sherehe ya kuaga mwaka mpya kwa Mabalozi na Wawakilishi wa mashirika ya kimataifa (New Year Diplomatic Sherry Party) iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, Kiongozi wa wanadiplomasia hao Mhe. Edzai Chimoyo ambaye ni Balozi wa Zimbabwe hapa nchini, ameahidi kuwa yeye na wenzake wapo tayari kutoa ushirikiano kwa Serikali ya Awamu ya Tano.
Pia amepongeza juhudi kubwa zilizofanywa kufufua Shirika la Ndege (ATCL) kwa kununua ndege mpya ambazo licha ya kurahisisha usafiri zitasaidia kukuza sekta ya utalii hapa nchini.
Akihutubia sherehe hizo, Rais John Magufuli amezialika nchi mbalimbali na wadau mbalimbali wa maendeleo kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kujenga uchumi wa viwanda utakaoiwezesha Tanzania kuingia katika nchi ya kipato cha kati.

Mhe. Dkt. Magufuli amesema ifikapo mwaka 2020 Tanzania imedhamiria uchumi wake ukue kwa wastani wa asilimia 10, sekta ya Viwanda iajiri asilimia 40 ya watanzania na pato la mtu kwa mwaka likue hadi kufikia wastani wa Dola 3,000 za kimarekani (sawa na Shilingi na takribani shilingi Milioni 6 na Laki 6 kwa mwaka)

Pia amewaomba wawahamasishe wadau watakaokuwa tayari kushirikiana na Tanzania katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi ikiwemo ujenzi wa reli ya kati yenye urefu wa Kilometa 1,200 kwa kiwango cha kisasa (Standard Gauge)kuanzia Dar es Salaam hadi Mwanza na Kigoma na kuunganisha hadi nchi za Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Rwanda,na kwamba tayari Serikali itaanza kujenga Kilometa 300 za kuanzia Dar es Salaam mwaka huu.
Kuhusu mwaka uliopita, Mhe. Rais Magufuli amesema Serikali imeanza kutekeleza awamu ya pili ya Mpango wa Maendeleo (2016-2021) uliopangwa kugharimu Shilingi Trilioni 107 ambapo kati ya fedha hizo Shilingi Trilioni 59 zitatolewa na Serikali ya Tanzania na kiasi kinachobaki kitatolewa na wadau mbalimbali wa maendeleo.
Mhe. Dkt. Magufuli amebainisha kuwa katika kutekeleza mpango huo, Serikali imechukua hatua ya kuongeza bajeti ya maendeleo kutoka asilimia 26 hadi kufikia asilimia 40 katika mwaka huu.

0 comments:

Post a Comment

Copyright © 2015 Dar One
| Distributed By Hotrootnews.blogspot.com