Sunday, September 25, 2016

SIMBA, YOUNG AFRICAN WAPEWA SIKU TATU TU......




Kamati ya Katiba, Sheria na Hadhi za wachezaji imetoa siku tatu kuanzia jana Septemba 24, 2016 kwa viongozi wa klabu za Simba SC na Young Africans SC kukaa chini na kumaliza suala la usajili wa mchezaji Hassan Ramadhani Kessy kwa njia ya mazungumzo ya kuelewana.

Hatua hiyo imefikiwa baada ya mjadala wa muda mrefu kuhusu kesi mbili zilizofunguliwa na Simba mbele ya kamati hiyo inayoongozwa na Mwanasheria Richard Sinamtwa. Kesi ya kwanza iliyofunguliwa na Simba SC ni dhidi ya Young Africans kudaiwa kuingia mkataba na mchezaji Hassan Kessy wakati bado ana mkataba na Simba SC.

Kesi ya pili ni Simba SC dhidi ya mchezaji Hassan Ramadhani Kessy kudaiwa kuanza kufanya mazoezi pia kusajili Young Africans na kwenda nje ya nchi wakati akiwa ndani ya mkataba na Simba SC. Kama hawatafikia mwafaka katika siku tatu walizopewa, mashauri hayo yatarudi mbele ya kamati na kufanya uamuzi kwa mujibu wataratibu, kanuni na sheria zinazoongoza mpira wa miguu Tanzania. Kupitia madai hayo, Simba inataka kulipwa dola 600,000 za Marekani.


Wakati huo huo, kamati imeondoa kifungo cha mwaka mmoja kwa mchezaji George Mpole wa Majimaji ya Songea baada ya klabu hiyo yenye maskani yake Mkoa wa Ruvuma kufikia mwafaka Kimondo FC.

 Pia kamati iliridhia mchezaji Enyina Darlington kutoka Nigeria kuanza kuitumika klabu yake baada ya kukamilisha vibali vya ukazi na kufanya kazi nchini vinavyotolewa na Idara ya Uhamiaji nchini katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

0 comments:

Post a Comment

Copyright © 2015 Dar One
| Distributed By Hotrootnews.blogspot.com