Friday, January 29, 2016

MANISPAA YA KINONDONI KUJENGA KIWANDA CHA TAKA NGUMU SH3.5 BILIONI



Dar es Salaam. Manispaa ya Kinondoni imepewa Sh3.5 bilioni za kujengea kiwanda cha kuchakata takataka ili kutengeneza mbolea baada ya meya wake kufanikiwa kuishawishi Halmashauri ya Mji wa Hamburg nchini Ujerumani.
Kiwanda hicho kitajengwa Mabwepande nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.
Akizungumza na wanahabari jana ofisi kwake, meya huyo kutoka Chadema, Boniface Jacob, ambaye alikuwa pamoja na mwakilishi wa mji wa Hamburg, alisema maandalizi ya ujenzi wa kiwanda hicho yataanza baada ya mwezi mmoja.
Alisema kwa siku Kinondoni inazalisha takataka tani 2,026 na zinazopelekwa dampo ni tani 700, huku 1,326 zikibaki katika maeneo mbalimbali, hivyo kiwanda hicho kitakuwa kinachukua tani 500 ili kupunguza wingi wa takataka hizo.
Katika mahojiano na gazeti hili mapema wiki hii, meya huyo alisema alifanya kazi kubwa ya kuushawishi mji huo kufadhili mradi huo.
Jacob ambaye pia ni Diwani wa Ubungo, alisema kiwanda hicho kitakamilika Juni mwakani na kutoa fursa ya ajira kwa vijana watakaokuwa wakikusanya takataka na wale watakaokuwa eneo la uzalishaji.
“Baada ya mwezi mmoja tunatarajia kuanza ujenzi huu. Kinondoni na Humburg ni kama kaka na dada, ndiyo maana walituambia tutafute ardhi na watasimamia gharama za ujenzi,” alisema Jacob.
Mwakilishi wa mji huo, Dk Florian Koelsch alisema halmashauri hiyo ina furaha kutekeleza mradi huo kwenye Manispaa ya Kinondoni, kutokana na uhusiano mzuri wa muda mrefu uliopo kati ya halmashauri hizo mbili.
“Malengo yetu ni mawili; la kwanza ni kupunguza takataka katika manispaa hii, pili ni kuhakikisha takataka hizi tunazozichukua zinazalisha mbolea itakayowasaidia wakulima wa Tanzania kuzalisha mazao yao kwa ufanisi,” alisema Dk Koelsch.     

0 comments:

Post a Comment

Copyright © 2015 Dar One
| Distributed By Hotrootnews.blogspot.com